HISTORY


VYUO VYA MAENDELEO YA WANANCHI - VMW (FCD’S)

Historia fupi ya Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi
Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi (VMW) ni “Taasisi za Kiserikali” ambazo zilianzishwa mwaka 1975 kutokana na wazo la Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius K. Nyerere, baada ya kutembelea nchi ya Sweden na kuona mfumo wa elimu isiyokuwa rasmi ulivyokuwa unaendeshwa na taasisi zinazojulikana kama Folk High Schools.
Vyuo ya Maendeleo ya Wananchi vilianzishwa kama sehemu ya awamu ya tatu ya Elimu ya Watu Wazima.  Hatua ya kwanza ilihusu kuondoa ujinga wa kutojua kusoma, kuandika na kuhesabu.  Hatua ya pili ilikuwa ya kuhakikisha kuwa mafanikio yaliyopatikana katika hatua ya kwanza yanakuwa endelevu na watu hawaurudii ujinga. Hatua ya tatu ilikuwa kuanzisha taasisi ambazo zingetoa maarifa na stadi kwa wananchi.  Aidha, uamuzi wa kuanzishwa VMW ulitokana na Waraka wa Baraza la Mawaziri No. 96 wa mwaka 1974 ambapo vyuo 25 vilianzishwa mwaka 1975 na kuendelea kuongezeka mwaka hadi mwaka kulingana na jinsi Wilaya mbalimbali zilivyo tambua umuhimu wa kuanzisha vyuo hivi. Hadi kufikia mwaka 1978, vyuo 53 vilikuwa vimeanzishwa.
Uanzishwaji wa VMW ulizingatiwa katika Sheria ya Elimu No. 25 ya mwaka 1978 chini ya Wizara ya Elimu. Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi vilipoanzishwa vilirithi majengo yaliyokuwa yakitumika kwa madhumuni tofauti tofauti vikiwemo Vituo vya Mafunzo ya Maendeleo Vijijini (Rural Training Centres) ambavyo vilianzishwa mwaka 1962, Vituo vya Mafunzo ya Wakulima (Farmers Training Centres) ambavyo vilianzishwa mwaka 1963, Shule za Kati (Middle Schools) ambazo zilianzishwa mwaka 1960 na Vituo vya Mafunzo ya Ushirika vilivyoanzishwa mwaka 1964. Vyuo pekee vilivyojengwa mahsusi kuitikia wazo la Baba wa Taifa la mwaka 1975 ni vinne, vyuo hivyo ni Sengerema, Ngara, Handeni na Bigwa, ambavyo vilijengwa mwaka 1975.

LENGO NA MADHUMUNI YA KUANZISHWA KWA VYUO VYA MAENDELEO YA WANANCHI (VMW)
Lengo Kuu
Lengo kuu la kuanzisha Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi lilikuwa ni kuimarisha maarifa na stadi kwa wananchi ili waondokane na ujinga, umaskini na maradhi na hatimaye kuleta maendeleo ya kiuchumi, kijamii, kisiasa na kiutamaduni. 
Madhumuni mahsusi yakuanzisha VMW
Madhumuni mahsusi ya vyuo hivi yameelezwa katika Waraka wa Serikali Na. 96 wa mwaka 1974 ambapo kipengele cha 5 kinaainisha madhumuni yafuatayo:
a)    Kumtayarisha Mtanzania ambaye ni mtu mzima aweze kukuza utu wake na kumfanya awe kamili katika jumuiya ya Watu wake;
b)   Kumtayarisha Mtanzania aweze kutumia akili zake vizuri na kuweza kuamua mambo  yake au ya Umma kwa njia iliyo sahihi;
c)    Kumsaidia Mtanzania aelewe siasa ya nchi yake na kumwezesha kushiriki kikamilifu bila woga au unafiki katika shughuli za siasa ya nchi yake;
d)    Kujenga moyo wa Mtanzania wa kushirikiana na wenzake katika shughuli au kazi za  nchi yake, na kuelewa umuhimu wa kuwa na uhusiano mwema na wenzake;
e)    Kumwezesha Mtanzania aweze kufikia kiwango cha juu zaidi katika ufundi wa kazi anazozifanya;
f)     Kumsaidia Mtanzania kukuza utamaduni wa Kitanzania; na
g)    Kuwafanya Watanzania wawe raia wenye manufaa katika Tanzania na dunia nzima.
Lengo na madhumuni haya yaliendelea kutekelezwa hadi mwaka 1987 ilipoundwa Tume ya Nsekela iliyoazinsha majukumu ya Wizara na Idara mbalimbali za Serikali. Tume ya Nsekela ya Februari 1987 ilibaini kuwa madhumuni na majukumu ya Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi yanashabihiana sana na yale ya Maendeleo ya Jamii ya kuwajengea uwezo wananchi ili wamudu majukumu yao vyema na kuboresha utendaji na maisha yao. Tume hiyo iliishauri Serikali kuhamishia VMW katika Idara ya Maendeleo ya Jamii.  Mwaka 1990, Serikali ilivihamishia VMW katika Idara ya Maendeleo ya Jamii chini ya iliyokuwa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Wanawake na Watoto. Ingawa lengo kuu halikubadilika, madhumuni yaliboreshwa ili kukidhi mabadiliko ya wakati huo katika jamii kwa kuzingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2025.

Madhumuni mahsusi yaliyoboreshwa
Madhumuni yaliyoboreshwa ni yafuatayo:
a)    Kuwapatia wananchi stadi mbalimbali za ujuzi na maarifa ambayo yatawasaidia kujiajiri na kuajiriwa hivyo kuondoa umaskini katika jamii;
b)   Kuwawezesha viongozi katika ngazi za Vijiji na Kata kuelewa majukumu yao na hivyo kusimamia kwa ufanisi utekelezaji wa sera mbalimbali za Serikali za kuondoa umaskini, kuwaletea wananchi maisha bora na kusimamia misingi ya utawala bora;
c)    Kuwezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika maamuzi, kutambua masuala ya jinsia, kuimarisha na kudumisha utamaduni wa kupiga vita mila na desturi zinazomkandamiza mwanamke katika jamii;
d)    Kuziwezesha jamii kuelewa umuhimu wa hifadhi, matumizi bora ya mazingira na kutumia rasilimali zilizopo kwa faida yao; na
e)    Kuziwezesha jamii kuelewa na kujikinga na janga la UKIMWI.

Majukumu ya Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi
Ili kufikia madhumuni tajwa hapo juu VMW vimepewa majukumu mbalimbali kupitia “Mwongozo wa Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi” wa mwaka 2002. Majukumu hayo ni pamoja na:
a)    Kutoa mafunzo yenye kuongeza maarifa, stadi na mbinu mbalimbali za kutatua matatizo halisi ya wananchi, ili wajiletee maendeleo kwa kutumia rasilimali zilizopo;
b)   Kutoa mafunzo yanayokidhi mahitaji halisi ya wananchi na soko;
c)    Kubuni na kuendesha miradi ya uzalishaji mali na utoaji huduma vyuoni na kuvisaidia vijiji vinavyozunguka vyuo. Aidha, miradi hii ifanyiwe uchambuzi na upembuzi yakinifu ili miradi inayotekelezwa iwe na taathira chanya kwa jamii;
d)    Kushirikiana na asasi na mashirika mbalimbali yanayotoa mafunzo, utaalam na rasilimali nyinginezo kuwaendeleza wananchi.  Katika zoezi hili, vyuo vitapata fursa ya kubadilishana uzoefu na asasi hizo;
e)    Kufanya utafiti wa mahitaji utakaotoa takwimu na taarifa sahihi zitakazotumiwa na vyuo, vijiji na mitaa, katika kubuni, kupanga na kutoa mafunzo ya ushirikishwaji, pamoja na kutekeleza miradi mbali mbali ya kujitegemea.  Aidha taarifa na takwimu hizo zinaweza kutumiwa na Halmashauri za wilaya, Miji, Manispaa na Jiji katika kuandaa mipango ya uwiano ya maendeleo;
f)     Kuwa vituo vya kufundishia, kutengeneza na kusambaza teknolojia na nyenzo za kurahisisha kazi wafanyazo wananchi;
g)    Kubaini mila zisizo za maendeleo na vikwazo vingine vya maendeleo katika maeneo vilipo vyuo na kutoa mafunzo dhidi ya vikwazo na mila hizo;
h)    Kubuni, kuandaa na kuendesha programu mbalimbali zitakazoinua kiwango cha fikra, maarifa na stadi  za wananchi kuhusu mazingira yao na ulimwengu kwa jumla;

i)     Kuendesha programu mbalimbali za hifadhi ya mazingira kwa wananchi zinazohusu matumizi bora ya ardhi kwa kuzingatia kanuni za kilimo na ufugaji bora, upandaji miti na maua na utunzaji wa vyanzo vya maji;
j)     Kuwashirikisha wananchi katika mijadala inayohusu masuala ya jinsia;
k)    Kubuni mikakati ya namna ya kuwafuatilia wahitimu kwa nia ya kupima kiwango cha taathira kilichofikiwa kutokana na mafunzo yanayotolewa vyuoni, matokeo ya upimaji huo yatatumika katika kurekebisha mitaala na mikakati ya utekelezaji; na
l)     Kushirikiana na asasi nyingine za Serikali, madhehebu ya dini mbalimbali na Mashirika yasiyo ya Kiserikali na Wananchi kubuni na kutekeleza programu na miradi madhubuti ya kutokomeza janga la UKIMWI na umaskini na kupiga vita rushwa.

SERIKALI KUBORESHA VYUO VYA MAENDELEO YA WANANCHI.
Serikali imesema kuwa itahakikisha inafanya maboresho katika vyuo vyote vya Maendeleo ya Wananchi hapa Nchi ili kuondoa adha mbalimbali zinazovikabili vyuo hivyo sambamba na kuondoa changamoto zinazowakabili wanafunzi vyuoni ikiwemo ya uchakavu wa majengo na miundombinu.
Hayo yamesemwa Bungeni Mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Afya, Maendeelo ya Jamii, Jinsia na Watoto Dkt. Hamisi Andrea Kigwangala wakati akijibu swali la Mbunge wa Nanyamba Abdallah Chikota aliyetaka kujua Serikali ina mpango gani wa kuboresha miundombinu na utoaji wa taaluma ya Chuo cha Maendeleo ya Wananchi (MTAWANYA) kilichopo Mkoani Mtwara.
Akijibu swali hilo Dkt.Kigwangala amesema kuwa Serikali ina mpango mkakati mpya wa kufanya maboresho katika vyuo vyote vya maendeleo ya Wananchi hapa Nchini ambapo kwa kipindi hiki Wizara ipo katika mazungumzo na Wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi ili kuweza kuvihamishia Kwenye Wizara hiyo ya elimu.
Aidha ameongeza kuwa lengo kuu la kufanya hivyo ni kuboresha mitaala inayotolewa katika vyuo hivyo lakini pia kuboresha utawala wa vyuo na kuongeza bajeti.

“Tunafahamu kero mbalimbali zinazovikabili vyuo vyetu vyote, tupo njiani kufanya baadhi ya marekebisho ili kuweza kuondoa kero hizo kwa wahusika” Alisema Kigwangala.

No comments:

Post a Comment